Wednesday 26 March 2014

Uwekezaji katika Kilimo cha zao la Mchikichi fursa iliyosahaulika Mkoani Kigoma






Michikichi ni zao mojawapo ya mazao ya mafuta ambalo hulimwa kwa wingi katika mikoa ya Kigoma, Mbeya na Tanga hapa nchini Tanzania. Aidha zao hili hulimwa pia kwa kiasi kidogo katika mikoa ya Kagera, Pwani, Rukwa, Morogoro na visiwa vya Pemba na Unguja.  Mkoa wa Kigoma ukiwa ni eneo muhimu kwa uzalishaji wa zao la michikichi hapa Tanzania kwa mwaka huzalisha zaidi ya tani 2,000 za mawese na zaidi ya tani 450 za mafuta ya mise.


Zao la mchikichi limekuwa mkombozi kwa wakulima wengi wa Mkoa wa Kigoma kwani hutumika kwa chakula, biashara, mafuta ya mise hutumika katika mapishi ya vyakula mbalimbali pia husaidia mwili kupata nguvu na joto na  hutumika katika utengenezaji wa sabuni na vipodozi mbalimbali.

Hata hivyo nchi za Indonesia na Malaysia ambazo zilitoa mbegu ya zao la mchickichi kutoka Mkoa wa Kigoma nchini Tanzania  miaka ya 1960 kwa sasa zinaongoza kwa uzalishaji na usambazaji wa mafuta ya mawese na bidhaa zitokanazo na michikichi.


Malysia pekee huzalisha tani milioni 18.79 million za mafuta ya mawese na kusambaza tani milion 18 za  mazao yanayotokana na zao la michikichi  duniani yakiwemo mafuta ya mawese ambayo Tanzania imekuwa ikiagiza takribani asilimia 65 ya mafuta ya mawese kutoka nchini ya Malaysia, zikifuatiwa na nchi nyingine kama Kolumbia na Thailand.
Kwa ukanda wa Afrika nchi za Nigeria, Kenya, Ghana, Cameroon na Benin zinatajwa kuongoza katika uzalishaji wa zao la mchikichi ambapo nchi ya Naigeria huzalisha tani milioni 2.3 ya mafuta ya mawese kwa mwaka na kuifanya kuwa nchi ya tatu kwa uzalichaji kidunia.
Matunda ya michikichi yakiwa yanaandaliwa kwa kukaushwa juani.

Kiasi hiki ni kingi ukilinganisha na fursa na uaptikanaji wa zao hili nchini Tanzania hususan Mkoa wa Kigoma  haipo katika rekodi ya uzalishaji. Sababu kubwa zinazofanya zao hili kutojulikana na hata kutomnufaisha mkulima wa kawaida nchini Tanzania ni teknolojia duni ya kilimo cha zao hili na ukosefu wa miunndombinu ya kuchakata mazao yatokanayo ya mchikichi hususan viwanda.

Kwa upande mwingine wataalamu wa kilimo hawajaweza kutilia maanana juu ya umuhimu wa zao hili, Serikali nayo haijawea kipaumbele namna ya kutoa ruzuku kwa wakulima wa zao la mchikichi ili waweze kujikwamua kiuchumi.
Wakulima wakiandaa matunda ya michikichi baada ya kuyatoa shambani.


Kadhalika bidhaa mathalani vile mapaa ya ndani (ruffing Materials) ambayo hutokana na makapi ya mchikichi huingizwa kwa wingi nchini kutoka Malaysia, na Afrika ya Kusini. Wakulima wa zao hili wengi hutumia zana duni katika kuchakata mazao ya michikichi kiasi ambacho hakiwapi tija kukuza uchumi. Sambamba na ukosefu wa zana za kilimo nguvu ya serikali kupitia wizara ya Kilimo ingeweza kufikiri namna ya kuwashirikisha wadau wa maendeleo, mashirika binafsi ili kushawishi uwekezaji katika zao la mchikichi kwa Kuweka miundombinu kama nishati ya umeme kwaajili ya kujenga viwanda. 
Moja ya njia za kiasili zinazotumika katika kuchakata na kuchuja mafuta ya Mawese mkoani Kigoma.

Kwakuwa zao hili hutoa malighafi zaidi ya tatu ingekuwa fursa kwa wakulima kutengeneza wigo wa upatikanaji wa biashara za mazao ya mchikichi kama vile vipodozi, vyakula vya mifugo, sabuni na mafuta ya kupikia na bidhaa nyingine nyingi kadha wa kadha.

Serikali kwa kutumia wataalamu wake katika ngazi mbalimbali ikiwemo Halmashauri, na ngazi mbalimbali za uongozi hazina budi kushirikiana na mashirika mbalimbali ya maendeleo katika kuhakikisha kuwa zao la michikichi linakuwa moja ya mazao makuu katika kukuza kipato na kuwaondolea umaskini wananchi wa mkoa wa Kigoma.

1 comment: