Thursday 26 January 2017

Mkoa wa Kigoma Wateketeza zana Haramu za Uvuvi

Jumla ya zana haramu za uvuvi 343 zenye thamani zaidi ya Shilingi za kitanzania 480,000,000 zimeteketezwa moto Mkoani Kigoma, ikiwa ni hatua ya Serikali ya Mkoa kupambana na Uvuvi usioendelevu.

Zana hizo zilikamatwa na vikosi vya doria ziwani kwa vipindi tofautitofauti katika ziwa Tanganyika Mkoani Kigoma.

Uvuvi wa Kutumia zana haramu katika Ziwa Tanganyika umekuwa tishio katika Mwambao wa Ziwa hilo ukiashiria kupoteza kabisa samaki na dagaa ambao ni kitoweo muhimu kwa wakazi wanaolizunguka Ziwa Tanganyika na kwingineko.

Akiongea wakati wa Zoezi la Uchomaji wa Zana hizo Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma Bw. Charles Pallangyo alisema zoezi hili ni endelevu kwani Mkoa wa Kigoma hautamvumilia Mtu yeyote kutumia zana za Uvuvi zisizo na tija katika kuendeleza Uvuvi endelevu.

Pallangyo amewataka wavuvi kufuata taratibu na sheria za matumizi ya zana za Uvuvi ili kulinda Rasilimali za Ziwa Tanganyika kuwa endelevu kwa faida ya Vizazi vijavyo.

Naye Afisa Uvuvi wa Mkoa wa Kigoma Bi. Ritta Mlingi amewatoa hofu wananchi wa Mkoa wa Kigoma kuwa hakuna samaki anayevuliwa kwa sumu kama ilivyokuwa inavumishwa na watu.

Aliongeza kuwa zana za uvuvi zinapokamata samaki hupandishwa mtumbwini saa hiyohiyo isipokuwa zana za “makila” ambazo huachwa hadi asubuhi ndipo huteguliwa na kupandishwa kwenye chombo.

Hivyo samaki wanaokamatwa mapema na “makila” hufa mapema kutokana na kukabwa sehemu za mapezi “Gills” , kasi yake kwa kuharibika huwa ni kubwa uizingatia wavuvu wengi hawana Barafu kwaajili ya kutunzia samaki ndani ya ziwa.

“Nawaomba wananchi wasiwe na wasiwasi kwani samaki hawanasumu isipokuwa kukosekana nyenzo bora za utunzaji pindi wanapovuliwa, hata hivyo mwanchi yeyote atakayekuwa na ushahidi wa samaki mwenye sumu anakaribishhwa kuleta usahidi huo katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa” aliongeza Mlingi.

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Brigedia Jenerali (Mst.) Mhe. Emannuel Maganga akiweka moto katika Nyavu na zana haramu za kuvulia zilizokamatwa katika Mkoa wa Kigoma

Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma Bw. Charles Pallangyo akiungana na Wadau mbalimbali katika zoezi la uteketezaji wa zana haramu za kuvulia samaki na dagaa Mkoani Kigoma



No comments:

Post a Comment