Thursday 18 April 2019

KONGAMANO LA KWANZA LA KIMATAIFA LA KIBIASHARA 'TANGANYIKA BUSINESS SUMMIT & FESTIVAL’


 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kigoma kwa kushirikiana wadau balimbali imeandaa 'Kongamano la Kwanza la Kimataifa la Kibiashara' maarufu kama 'Tanganyika Business Summit & Festival’. Kongamano hili la kwanza na la aina yake litafanyika Mkoani Kigoma kwa siku tatu kuanzia tarehe 9 mpaka tarehe 11 Mei, 2019 katika ukumbi wa mikutano wa NSSF. Mgeni rasmi katika Kongamano hilo atakuwa ni Mhe. Samia S. Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kongamano lina lengo la kuwakutanisha wafanyabiashara wa Mkoa wa Kigoma na Tanzania kwa ujumla na wafanyabiashara wa nchi jirani za Burundi, DRC Kongo, Zambia, na Rwanda ili kwa pamoja kujadili na kuafiki namna ya kukuza biashara na uwekezaji kutokana na fursa zilizopo ndani ya nchi hizi hususan kwenye sekta za viwanda, kilimo, mifugo, uvuvi, usafirishaji na biashara kwa ujumla. Kongamano hili litaleta manufaa mengi kwa Mkoa,Washiriki na Nchi kwa ujumla ikiwemo:-
1.    Kutangaza fursa za biashara na uwekezaji baina ya nchi majirani
2.  Kuwakutanisha wafanyabiashara/wawekezaji wa nchi washiriki ili kubainisha fursa mbalimbali za kibiashara na uwekezaji zitakazowezesha kuanzisha na kuendeleza miradi katika sekta za viwanda, kilimo, mifugo, uvuvi, usafirishaji, na biashara kwa ujumla.
3.  Kuanzisha mahusiano ya kibiashara na muingiliano wa kibiashara baina ya nchi za Maziwa makuu za Tanzania, Burundi, Rwanda, Zambia na Demekrasia ya  Kongo.
4.  Kuimarisha biashara za mipakani
5.  Kujenga mazingira mazuri ya biashara na uwekezaji baina ya nchi majirani
6.  Kujenga muingiliano wa wajasiriamali na wawekezaji au wafanyabiashara wakubwaa
7.  Kujenga  moyo na tabia za ujasiriamali miongoni mwa vijana na wanawake wa mkoa wa Kigoma
8.  Kujenga mahusiano ya kudumu baina ya taasisi za serikali,na sekta binafsi miongoni mwa nchi wanachama
Watanzania kutoka Mikoa yote wanaalikwa kuchangamkia fursa hii kwa kushiriki kongamano ili kunufaika na fursa mbalimbali zitakazojitokeza ikiwa ni pamoja na kunadi fursa za uwekezaji na biashara za mipakani, kujifunza mbinu mpya za biashara na uwekezaji kutoka kwa washiriki sambamba na kutafuta wabia, masoko, mitaji na teknolojia mpya.
Kongamano linatarajiwa kuwa na washiriki zaidi ya 300 na litaambatana na maonesho (Exhibition) ya bidhaa na huduma mbalimbali kutoka Tanzania, Burundi; DRC Kongo, Rwanda na Zambia.




No comments:

Post a Comment