Thursday 26 January 2017

Zaidi ya silaha haramu 5600 zimeteketezwa moto Mkoani Kigoma


Zaidi ya silaha haramu 5600 zimeteketezwa moto Mkoani Kigoma ikiwa ni moja ya hatua za Serikali katika kupambana na uzagaaji wa silaha haramu nchini.

Akiongoza zoezi la uteketezaji wa silaha hizo Waziri wa Ulinzi na Mambo ya Ndani ya Nchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mwigulu Lameck Nchemba alisema “tatizo la uzagaaji wa silaha ni la kidunia, kwa kiwango kikubwa uzagaaji wa silaha hovyo umeathiri maendeleo kiuchumi, kisiasa na Kijamii”

Aidha ameongeza kuwa tangu Januari 2017, amefuta ukimbizi wa Makundi kama ilivyokuwa awali na utaratibu utakuwa kila Mkimbizi ataingia nchini baada ya kuhojiwa na kujadiliwa na Kamati husika.

Alitoa rai kwa Watazania wote wanaomiliki Silaha kinyume na taratibu za nchi kuzisajili au kuzisalimisa silaha hizo, na mwisho wa zoezi hilo itakuwa tarehe 30 Juni, 2017, baada ya hapo hatua kali za watakaobainika zitachukuliwa.

Silaha zilizoteketezwa zilikamatwa kutoka katika Mikoa ya Mara, Mwanza, Simiyu, Shinyanga, Tabora, Katavi, Rukwa, Kagera na Kigoma.

Hata hivyo Mkoa wa Kigoma umetajwa kuongoza kwa uzagaaji wa Silaha haramu kwa asilimia zaidi ya 40%  na matukio yanayohusisha silaha kwa 20 % ukiligaishwa na Mikoa Mingine.

Akizungumza katika zoezi la Uteketezaji wa Silaha hizo Kamishna wa Oparesheni na Mafunzo Nsato Marijani Msanzya alisema Mkoa wa Kigoma unaogoza kutokana na kupakana na nchi zenye machafuko ya Kisiasa, kupokea wakimbizi wengi  ambao huingia kwa makundi bila kupekuliwa, baadhi yawakimbizi wasio waaminifu hutumia mwanya wa ukimbizi vibaya kwa kufanya matendo mengi ya kihalifu.

Hadi sasa wakimbizi waliopo Mkoani Kigoma ni zaidi ya 27,000 ambao ni chimbuko la uzagaaji wa silaha haramu Mkoani Kigoma. Imeelezwa kuwa katika Mkoa wa Kigoma kwa siku hupokea wakimbizi 400 hadi 500 wakitokea Nchi jirani za Burundi na Congo.

Hata hivyo taarifa  zinasema wengi wao sasa hawakimbi kwa hofu ya machafuko ya kisiasa bali wanakimbia njaa na ugumu wa maisha nchini mwao.

Naye Naibu Kamishna wa Polisi Sekretarieti ya Umoja wa Kikanda wa Kushughuliikia uzagaaji wa silaha Bw. Theonest Mshindashaka alisema Jumla ya Silaha zilizokwisha kuteketezwa kati ya 2014 hadi 2017 ni zaidi ya 17,000.

Uteketezaji wa silaha haramu umefadhiliwa na Serikali ya Marekani Kitengo cha Kupambana na Uzagaaji wa Silaha.

Silaha mbalimba za moto zipatazo 5608 zikiwa zimeandaliwa tayari kwa Kuteketezwa katika Uwanja wa Lake Tanganyika Mkoani Kigoma


Waziri wa Ulinzi na Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Mwigulu Lameck Nchemba (MB) akiteta jambo na Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Mhe. Brigedia Jenerali (Mst.) Emannuel Maganga muda mchache kabla ya kuteketeza Silaha haramu.


Waziri wa Ulinzi na Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Mwigulu Lameck Nchemba (MB) akiwasha moto Silaha haramu kupitia Mfumo maalumu wa ulipuaji



Habari zote na

G.D. Ng'honoli

  Afisa Habari na Mawasiliano wa Sekretarieti ya Mkoa wa

 Kigoma

No comments:

Post a Comment